Jumatano, 2 Aprili 2014

NAFASI YA FAMILIA KATIKA MAKUZI YA MTOTO..

FAMILIA ina nafasi kubwa sana katika ukuaji wa mtoto mpaka anapofikia umri wa kupevuka. Wazazi hususan mama ndio wanaokuwa wa kwanza kuwaathiri watoto kutokana na ukaribu baina yao. Watoto wengine ambao hucheza nao wana nafasi inayokaribiana na ile ya wazazi. Hii inaweza kuonekana kwa watoto wa miaka mitatu na zaidi ambao huongea kama wazazi wao au watoto wengine wanaocheza nao.

Moto wa miaka 4-5 anapompiga mwenzake huiga yale ambayo yeye pia anafanyiwa. Au anaona yanafanyika. Mtoto huyu anapoulizwa au kukatazwa juu ya kumpiga mwenzake jibu lake huwa "mbona yeye kanipiga" au "mbona wewe ulinipiga?"

WANAPOFIKIA umri wa kwenda shule, uhusiano kati yao na watoto wengine na wazazi hubadilika kwa kiasi kikubwa. Hii inatokana na mabadiliko ya kiakili yanayoendelea kwa mtoto. Katika kipindi hiki wanakuwa mahiri zaidi na wanauwezo zaidi wa kujidhibiti, hivyo wazazi wanaanza kuwapa majukumu zaidi, mara nyingi ni pamoja na kuwashirikisha katika kazi za ndani. 

Wakati huo huo, wazazi hubadilisha namna ya kuwalea ambapo wanatumia nguvu kidogo kama vile ukali, adhabu n.k. na hutumia mbinu za kushughulisha akili ili kuwafanya watoto kutenda kulingana na kanuni na maadili. Kwa utaratibu huu mfumo wa uhusiano unakuwa wa kurekebishana. Mtoto hurekebisha tabia na matendo yake ili yaendane na maelekezo ya mzazi na mzazi pia kwa upande wake hujirekebisha ili asitumie nguvu katika kumwelekeza mtoto. Kwa mfano wakati mzazi anapomwelekeza mtoto namna ya kuvaa shati na kufunga vifungo humlazimu kutumia lugha ya upole na ya taratibu ili mtoto aelewe na afuate anayoambiwa.

Badala yake anapotumia ukali na kuongea maneno mengi huku akiwa amekasirika mtoto huweza kujifunza woga na kutojiamini na ukaidi na kutojali.
 


Aina za malezi na athari zake.

Kuna aina nyingi za malezi kama ambavyo tulivyo na wazazi wa aina nyingi, wazazi hawa wana namna tofuati ya kulea watoto kulingana na wanavyoona kuwa ni bora kwa watoto wao. Hata hivyo tutaangalia makundi mawili na athari zake katika makuzi ya mtoto. 

(i) Kiwango cha huruma kulinganisha na ukatili 

(ii) Kumdhaibiti mtoto na kumpa nafasi. 

Kabla hatujaendelea ni muhimu tujue kuwa, mgawanyo huu unaonesha uhusiano uliopo baina yake na tabia ya mtoto. Kwa mfano wazazi ambao ni wapole na wenye mapenzi na wanatumia mbinu ya kufikirisha katika kurekebisha tabia ya mtoto, wanakuwa na watoto ambao ni wenye ushirikiano, wanaelewa na kushika desturi na maadili na wanawajibika kwa vitendo vyao. Mtoto aliyelelewa katika familia ya namna hii ataelewa taratibu na maadili yanayofuatwa na yeyemwenyewe kuyafuata na inapotokea ametenda kinyume na anavyotakiwa kutenda anajua kosa na kulikubali na hatimaye kuomba radhi kwa aliowakosea. 

Uchangamfu wa wazazi kwa watoto unahusiana na tabia za watoto hao katika kushirikiana na watu wengine. Pia uchangamfu husaidia kuondoa matatizo ya kinidhamu, kukosekana kwa uchangamfu na mapenzi kwa watoto, na badala yake kutegemea ukali, kugombeza, kuadhibu kunasababisha tabia ya kuharibu vitu na kutosikia na kutotii. Vile vile watoto huwa na tabia ya kuwaona watu wengine kuwa ndio chanzo cha matatizo yao mfano anapoadhibiwa baada ya kufanya kosa fulani, mtot huyo humuona aliye muadhibu kuwa ni mwoneaji,hapendi maendeleo yake nk. 

Kwa upande wa kundi la pili tunaona kuwa, tabia ya kuzuia watoto kufanya kila kitu huweza kusababisha woga na wasiwasi. Watoto huweza kuwa wapole na watiifu, hii inaweza kuonekana machoni mwa wazazi kwamba ni kitu kizuri lakini watoto hawa huweza kuwa na tabia ya kuwa na aibu kupita kiasi, kuwa na wasiwasi na kujifikiria walivyo ili wasionekane na makosa. Watoto hawa pia hushindwa kujitegemea katika mambo mbalimbali na wanakuwa hawawezi kujiamini katika kufanya jambo wao wenyewe. 
Hata hivyo kuwa wapole kupindukia kwa watoto na kuruhusu bila mpaka husababisha watoto hukosa adabu. 

Watoto siku zote wanakuwa vile tunavyowafanya wawe na katu hawawi kinyume chake. Wazazi wanapolalamika juu ya tabia fulani mbaya ya watoto wajue tu kuwa sehemu kubwa ya ubaya huo unatoka kwao. Ukweli uko wazi kwamba "hakuna mwanamke duniani aliyewahi kuzaa mtoto mbaya", ubaya wa watoto wetu tunawapa wenyewe! 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni