Ijumaa, 23 Mei 2014

NINI CHA KUFANYA MARA TU MTOTO ANAPOLIA.



Hatua anazopaswa kuzichukua Mama mara tu mtoto anapolia.

Kuna vitu ambavyo mzazi unaweza kufanya ili kumpa faraja mtoto wako pindi anapolia. Yawezekana baadhi ya mambo yatakayoshauriwa hapa yasiwasaidie watoto wote, hivyo basi mzazi ama mlezi ni vizuri ukamjua mtoto wako na kufahamu kwa undani ni kitu gani hasa kinachoweza kusaidia kumtuliza.

1. Kumbeba mtoto
Watoto wachanga huonyesha upendeleo fulani wa hisia, kama vile walivyokuwa ndani ya tumbo, hivyo basi unaweza kujaribu kumvingirisha mtoto wako katika blanketi au nguo zozote za kumbebea kama khanga au vitenge ili kuona kama atapenda hali hiyo.

Watoto wengine hawapendi kuvingirishwa kwenye blanketi na hupenda aina nyingine ya kupata faraja kama vile kubebwa. Wapo wazazi wanaopenda kumbeba mtoto kiasi cha kumfanya mtoto asikie mapigo ya moyo, kitendo ambacho humpa faraja sana mtoto.



2. Kumwimbia nyimbo au sauti za kumbembeleza
Akiwa tumboni mwa mama, mara kwa mara mtoto alikuwa akisikia mapigo ya moyo ya mama. Hali hii ndiyo sababu kubwa ya watoto wengi kupendelea kubebwa na mama zao.

Hata hivyo kuna aina nyingine za sauti zinazoweza pia kusaidia kumtuliza mtoto. Mzazi ama mlezi unaweza kujaribu kuweka muziki wa taratibu au kumuimbia mtoto nyimbo za kubembeleza kwa sauti ya chini sana.

Unashauriwa kutokuweka miziki ya haraka au yenye sauti kubwa kwa sababu inaweza kumwondolea hali yake ya utulivu na hivyo kumfanya ashindwe kuacha kulia.

3. Jaribu kumkanda au kumsugua taratibu (masaji)
Kumkanda kanda au kumsugua mtoto taratibu mgongoni au tumboni kunaweza kumsaidia sana kumfariji mtoto. Iwapo inaonekana mtoto anapata tabu wakati wa kubeua au kucheua, jaribu kumlisha akiwa wima zaidi na kila baada ya kumlisha mweke juu ya bega lako na kumsugua taratibu mgongoni ili kumsaidia atoe gesi kwa kubeua.

Baadhi ya watoto ambao wana “colic” wakati mwingine hutulia hasa wanaposuguliwa taratibu tumboni na hii huweza kuwafanya wajisikie vizuri kwa vile huihisi kwamba angalau mzazi ama mlezi unajitahidi kufanya kitu fulani kusaidia kumwondolea shida yake.

4. Mpatie kitu cha kunyonya
Kwa baadhi ya watoto waliozaliwa, haja ya kunyonya ni kubwa sana na hivyo kumpatia chuchu safi iliyotengenezwa kwa ajili hiyo au kidole kisafi cha mama inaweza kuleta faraja kubwa kwao. Kunyonya kutamsababishia mapigo ya moyo wake kuwa katika kiwango chake cha kawaida, kupumzisha tumbo lake, na kutulia.

Ulezi wa watoto wachanga ni kitu kigumu lakini ulezi wa mtoto ambaye hulia mara kwa mara ni ngumu zaidi. Kupata msaada na kuungwa mkono wakati unapohitaji msaada ni muhimu zaidi.

Mzazi hana budi kufahamu kuwa kwa jinsi siku zinavyopita, na kwa kadri mtoto anavyokua, mtoto anajifunza njia mpya ya kuwa na uwezo wa kuwasilisha mahitaji yake na hivyo ni muhimu mzazi naye kujifunza njia hizo ili kumuwezesha kumpatia mtoto mahitaji yake anayohitaji kwa haraka na wakati unaostahili.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni