Sababu zinzo mfanya mtoto kulia .
Ni kawaida kwa watoto kulia. Hata watoto
wanaozaliwa na afya njema kabisa wanaweza kulia kwa jumla ya wastani wa kati ya
saa moja mpaka matatu kwa siku. Kwa vile watoto hawawezi kujifanyia chochote
wao wenyewe zaidi ya kutegemea wazazi, walezi ama watu wengine wanaowazunguka
katika kuwapatia chakula, joto, na faraja, kilio ni njia ya mtoto ya
kuwasilisha moja ya mahitaji hayo.
Kama mzazi mpya, wakati mwingine inakuwa
vigumu kutambua mtoto wako anahitaji nini anapolia. Mzazi anaweza kuwa na
maswali kadhaa kichwani mwake, je, mtoto ana njaa, anasikia baridi, ana kiu,
anaumwa ama amechoka?
Katika siku za mwanzo, hali ya namna hii inawawia vigumu
wazazi wengi, wasijue nini la kufanya. Hata hivyo, kwa kadiri siku zinavyopita
mzazi mpya ataweza kutambua kuwa kilio cha mtoto wake kinamaanisha anahitaji
nini kutokana na mfumo wake wa kulia.
Kadiri watoto wanavyokua ndivyo ambavyo
hujifunza hatua mbalimbali za kuwasiliana na wazazi ama walezi wao. Wanakuwa na
namna nzuri ya kuwasiliana kwa mfano kwa macho, na kutoa sauti, na hata
kutabasamu ambavyo vyote kwa pamoja hupunguza haja ya kulia.
Sababu
zinazofanya watoto kulia
Tuangalie sababu kadhaa zinazosababisha mtoto
kulia na nini anachotakiwa mzazi ama mlezi kufanya pindi mtoto anapolia.
1. Hitaji la chakula
Njaa ni mmoja ya sababu kubwa inayowafanya
watoto wengi kulia. Uwezekano wa mtoto kulia unaendana sana na umri wa mtoto.
Kadiri jinsi mtoto alivyo mdogo zaidi ndivyo uwezekano wa kulia sana pindi
anapohisi njaa unavyokuwa mkubwa, isipokuwa katika siku mbili za mwanzo baada
ya kuzaliwa ambapo watoto hula kwa kiasi kidogo sana.
Kwa kawaida katika siku
mbili za mwanzo tangu mtoto kuzaliwa, maziwa ya kujilimbikizia mapema sana
yaani ‘colostrum’ huwa ni kidogo sana kwa mama walio wengi na huanza kuongezeka
kuanzia siku ya tatu baada ya kujifungua.
Pia tumbo la mtoto katika kipindi
hiki huwa bado dogo sana na hivyo uwezo wake wa kuhifadhi maziwa anayonyonya
huwa bado mdogo hali ambayo humfanya mtoto kujisikia njaa.
Hivyo kama mtoto
wako analia, uwezekano mkubwa ni kuwa ana njaa na hivyo mzazi unashauriwa
kumnyonyesha. Inawezekana mtoto asiache kulia mara moja, lakini mama
unashauriwa kuendelea kumnyonyesha taratibu na mtoto anaweza kuacha kulia kwa
kadiri anavyoburudika na chakula na kuanza kushiba. Iwapo mama unadhani mtoto
wako ameshiba lakini bado anaendelea kulia, inawezekana kuna sababu nyingine
zaidi.
2. Hitaji la starehe
Baadhi ya watoto wanakuwa na hisia kali pindi
vitu kama nguo inapoelekea kumbana sana au iwapo anahisi kuna kitu chochote
ndani ya nguo yake kinachomsababishia maumivu.
Wapo baadhi ya watoto ambao
hawaoneshi kuhangaika pale nepi zinapokuwa zimelowa sababu ya mkojo au kinyesi,
kwa vile baadhi yao huihisi joto na hivyo kupendezewa na hali hiyo, wakati
watoto wengine hulia na kuhitaji kubadilishwa nguo walizovaa mara moja, hasa
kama ngozi zao laini zinasumbuliwa.
Ni vyema kwa mzazi ama mlezi kumchunguza
mtoto wako kama amechafua nepi na kumbadilisha. Vilevile ni vyema kuangalia
kama nguo alizovikwa hazibani na hakuna chochote ndani ya nguo kinachomletea
maumivu.
3. Hitaji la kuwa na joto la wastani
Baadhi ya watoto hawapendi kubadilishwa nepi
au kuogeshwa. Hawajazoea kuhisi hewa yenye joto tofauti juu ya ngozi zao. Wengi
wao hupendelea sana kuwa na hali ya jotojoto lililohifadhiwa. Kwa hiyo ni vyema
kumbadilisha mtoto nepi haraka ili kuweza hifadhi joto lake.
Inashauriwa pia
kutokumvalisha nguo nyingi zaidi ya mahitaji ili mtoto asije akahisi joto zaidi
ya analolihitaji mwilini na hivyo kupelekea kuanza kulia.
Inashauriwa pia kutomfunika mtoto kwa mashuka
au mablanketi mengi hasa wakati wa kumlaza.
Kabla ya kuamua ni kiasi gani cha
nguo unachohitaji kumfunika mtoto wakati wa kulala, ni vyema kuangalia kama
mwili wa mtoto ni wa moto au baridi isivyo kawaida. Unaweza kufanya hivi kwa
kuhisi joto la tumbo lake kwa kutumia kiganja chako.
Iwapo mtoto ana joto sana,
unashauriwa kupunguza idadi ya nguo za kumfunika vivyo hivyo iwapo unahisi
mtoto ana baridi isivyo kawaida inashauriwa kuongeza idadi ya nguo za
kumfunikia.
Usipime joto la mwili wa mtoto kwa kutumia joto la mikono au miguu
yake kwani si kitu cha uhakika na mara nyingi huleta matokeo yasiyo sahihi kwa
vile ni kawaida ya mikono au miguu ya watoto kuwa ya baridi.
4. Hitaji la kushikwa ama kubebwa
Baadhi ya watoto wanahitaji kuwa karibu na
wazazi wao kwa kubebwa na kubembelezwa. Watoto wakubwa wanapata faraja kwa
kuwaona wazazi wao wakiwa karibu na kusikia sauti zao, lakini mara nyingi
watoto wachanga wanahitaji kushikiliwa na kubembelezwa kwa faraja.
Kama
umemlisha mtoto wako na kumbadilisha nepi wakati mwingine mtoto anahitaji
kubebwa pia.
Baadhi ya wazazi uhofia kuwa wanaweza
kuwaharibu watoto wao kimakuzi pindi wanapowabeba sana. Hiyo si kweli hususani
kwa miezi michache ya mwanzo tangu kuzaliwa kwa mtoto.
Wakati baadhi ya watoto
hawapendi kubebwa, wapo wengine ambao hutaka kubebwa karibu muda mwingi. Iwapo
mtoto wako ni wa namna hiyo, unaweza kumbeba mgongoni au kwa jinsi yeyote ile
ambayo itakuruhusu kuendelea na shughuli zako nyingine.
5. Hitaji la mapumziko
Ni rahisi kudhani kuwa mtoto atapata usingizi
wakati wowote popote pale alipo. Hata hivyo, kwa baadhi ya watoto, hali kama za
ujio wa wageni, kelele au hali ya fujo zinaweza kumfanya mtoto kusisimka na
hivyo kuwa vigumu kwake kutulia.
Watoto wachanga wanaweza kupata ugumu wa
kukabiliana na mambo ya kusisimua sana kwa mfano vitu kama taa, kelele, au
kubebwa kwa kupokezana kutoka kwa ndugu au mgeni mmoja mpaka mwingine hasa
wanapokuja kumtembelea mama.
Hali hii humfanya mtoto kushindwa kustahamili na
hivyo kuzidiwa na hayo yote. Wazazi wengi wamegundua kwamba watoto wao hulia
zaidi kuliko kawaida wakati ndugu au jamaa wakiwatembelea hususani nyakati za
jioni. Kama hakuna sababu nyingine maalum inayopelekea mtoto wako kulia,
yawezekana basi kilio chake kinasababishwa na uchovu.
Mzazi ama mlezi
anashauriwa kumpeleka mtoto sehemu tulivu iwe chumbani au sehemu nyingine
ambapo patamwondolea hali ya kusisimuliwa na hivyo kumfanya aweze kuacha kulia
na kupata usingizi.
6. Hitaji la kitu cha kumfanya mtoto ajisikie
vizuri
Iwapo umemlisha mtoto wako na kuhakikisha kuwa
yupo vizuri lakini akawa bado anaendelea kulia, mzazi ama mlezi unaweza kuwa na
hofu kuwa mtoto ni mgonjwa au ana maumivu. Ni vigumu sana nyakati za mwanzo kwa
mzazi kutambua kuwa mtoto wake analia kwa sababu ya kutokuwa na furaha au kuna
kitu kinachomuumiza.
Mtoto ambaye ni mgonjwa mara nyingi hutoa sauti ya kilio
kilicho tofauti na sauti yake ya kawaida. Sauti hii inaweza kuwa ya haraka
zaidi au kali sana. Vile vile kwa mtoto ambaye amezoea kulia mara kwa mara,
pindi anapoonesha hali ya utulivu isiyo ya kawaida inaweza kuwa dalili ya
kwamba ni mgonjwa. Jambo muhimu la kukumbuka ni kwamba hakuna mtu anayemjua
mtoto wako vizuri zaidi kuliko wewe.
Kwa hiyo basi kama mzazi ama mlezi unahisi
kwamba kuna kitu tofauti kwa mtoto wako ni vyema ukaonana na wataalimu wa afya.
Wataalamu wa afya daima watayachunguza matatizo ya mtoto wako kwa umakini
mkubwa na hivyo kujua sababu ya mtoto kulia. Mzazi ama mlezi unashauriwa
kuonana na daktari iwapo mtoto wako ana shida ya kupumua pindi anapolia, au
kama kulia kwa mtoto kunaambatana na kutapika, kuharisha ama kutopata choo.
7. Mtoto anahitaji kitu, lakini hujui ni nini
Wakati mwingine unaweza kushindwa kufahamu ni
nini kinachomsababishia mtoto wako kulia. Wakati mwingine watoto wanakosa
furaha. Hali hii ya kukosa furaha bila sababu inaweza kudumu dakika chache au
saa kadhaa ambapo mtoto huendelea tu kulia mara kwa mara.
Wakati mwingine
baadhi ya watoto hulia kwa muda mrefu huku wakirusha rusha miguu. Hii hali
yaweza kusababishwa na maumivu ayapatayo mtoto kwenye tumbo. Kwa kitaalamu hali
hii hujulikana kama colic.
Huwa vigumu sana wazazi wengi kukabiliana na
mtoto ambaye ana colic. Hakuna tiba ya uchawi kwa colic, aidha ni mara chache
sana hali hii inadumu kwa zaidi ya miezi mitatu. Hata hivyo ni vyema kupata
ushauri wa daktari pindi unapohisi mtoto wako ana colic.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni